Kilindi kuanzisha viwanda vya kuongeza thamani zao la mahindi


Katika kukabiliana na tatizo la njaa pamoja na ulanguzi wa mazao ya nafaka unaofanywa na wafanyabishasha walanguzi Halmashauri ya wilaya ya Kilindi imeanza mchakato wa ujenzi wa viwanda vya kusindika mazao ya Mahindi na Mtama ili kuyaongezea thamani.

Hayo yamebainishwa mwishoni mwa wiki na Mkurugenzi Mtendaji wa halmshauri hiyo, Daudi Mayeji wakati akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa miradi ya kuleta matokeo makubwa sasa wakati wa mkutano wa pamoja (Inter Council Meeting) wa siku mbili uliofanyika wilayani handeni na kujumuisha viongozi wa kisiasa na watendaji wa ngazi ya mkoa na halmashauri.

Alisema hatua hiyo itapunguza tatizo la njaa linalozikabili kaya kila mwaka, itaongeza kipato cha mkulima kutokana na kuongezeka kwa thamani ya bidhaa za unga wa mahindi na mtama sokoni ambao utakasindikwa viwandani na wakulima.

“Mradi huu umetokana na uchunguzi wetu tuliofanya na kubaini kwamba wakati wa mavuno wakulima wanapata mengi lakini yanachukuliwa kwa bei ndogo na wafanyabishara walanguzi kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania na nje ya nchi na hivyo baada ya muda mfupi wao hubaki maskini wa kuomba chakula cha msaada”, alisema na kuongeza.

“Kwa hiyo tukaona tuwe na viwanda vya kusindiaka na kufungasha unga wa mahindi na mtama ambavyo vitasimamiwa na wakulima wenyewe kupitia chama chao cha ushirika lengo la halmashauri ni kuhakikisha mkulima wa kilindi anapata tija kupitia shughuli zake hizo”.

Alisema ili kuhakikisha uzalishaji wa kutosha wa mazao hayo tayari wameanzaisha program maalum ya kuwafundisha wakulima hao mbinu za kisasa za uzalishaji wa mazao hayo na kwamba tayari wakulima wa kata ya Songe wametenga eneo la ujenzi wa kiwanda chao.

“Mradi huu utakwenda kwa awamu na tayari tumehamasisha wakulima wanajiunga kwenye vyama vya ushirika kwa kutoa viingilio na hisa na tumeshatembelewa na taasisi za fedha ambapo kwa kuanzia kata ya Songe wamepata wazalishaji ambao wataleta mashine yenye uwezo wa kusindika tani 20 za mahindi kwa siku”, alisema.

Mayeji alisema mashine moja ina thamani ya sh. Milioni 200 na inaundwa na sehemu kuu nne ambazo ni kwa ajili ya kusafisha nafaka, kukoboa, kusagwa na kisha kufungashwa katika vifungashio maalum na kwamba katika kufanikisha kiwanda hicho cha awali halmashauri imechangia kiasi cha sh. Milioni 93 kwa ajili ya ununuzi wa mitambo.


Written by

0 comments: