RC Tanga Ashauri Chanjo Ya Surua Na Rubella Kwa Watoto Haina Madhara Kwa Binadamu Ni Kinga Kwa Afya Bora


Mkoa wa Tanga kama ilivyo kwa Mikoa mingine ya Tanzania iko kwenye maandalizi ya  kampeni shirikishi ya chanjo ya Surua na Rubella. Maandalizi hayo ni pamoja na kuelimisha na kuhamasisha wakazi wote wa Tanga kwa ngazi ya Mkoa, Wilaya,Tarafa, Kata,Vitongoji na vijiji kujitokeza kwa wingi na kuwapeleka watoto wao katika vituo vya afya tarehe 18 hadi 24 Oktoba ili kupata chanjo ya magonjwa hatari ya Surua na Rubella.
Sambamba na chanjo ya Surua na Rubella kwa watoto wenye umri wa miezi tisa (9) na chini ya miaka 15, zoezi hilo la chanjo linalenga kutoa vidonge vya vitamin A kwa watoto wote wenye umri wa miezi 6 mpaka miezi 59 , dawa za minyoo,  kwa watoto wote wenye umri wa miezi 12 hadi miezi 59 na dawa za matende na mabusha  kwa watoto miaka mitano (5) na kuendelea .
Akizungumza wakati wa kufungua kikao cha wadau wa afya (PHC) kilichofanyika  leo katika ukumbi wa mikutano wa ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Chiku Gallawa, Mkuu wa Mkoa wa Tanga ametoa wito kwa wadau wote wa Afya Mkoani Tanga kuweka jitihada za kuhakikisha Mkoa wa Tanga unaendelea kufanya vizuri katika zoezi la Chanjo.
 Mkoa wa Tanga ambao kwa takribani miaka mitatu mfululizo umeendelea kufanya vizuri katika utoaji chanjo kwa ngazi ya kitaifa kwa kushika nafasi ya kwanza, umejiwekea mikakati mizuri ya kutoa elimu na hamasa kwa wazazi kuhakikisha wanawapatia watoto wao chanjo muhimu.
“Ndugu washiriki, nashauri tujipange kutoa elimu na hamasa kwa wananchi wetu walio katika maeneo yetu ili waweze kujitokeza kwa wingi katika zoezi la Chanjo. Jitihada ziwekwe katika kuwaelimisha kuwa chanjo hizi hazina madhara yeyote kwa binadamu badala yake ni kinga kwao.”amesisitiza Mhe. Gallawa.
Naye mwakilishi kutoka Wizara ya Ustawi wa Jamii Dr. Maduhu amesema Wizara yake imejipanga vyema katika kusambaza vifaa tiba na elimu kwa wahudumu ili kuhakikisha zoezi hilo linaenda vizuri.
Kampeni ya chanjo kitaifa itaanza  rasmi tarehe 18  hadi 25, Octoba na kauli mbiu ya mwaka huu ni “Linda , Okoa Maisha Zuia Ulemavu – Kamilisha Chanjo
 Dr. Maduhu  Mwakilishi kutoka Wizara ya Afya na Ustawi wa jamii akieleza juu ya jinsi wizara yake ilivyojiandaa kukamilisha zoezi la chanjo Mkoani Tanga. kulia ni Mkuu wa Mkoa wa tanga Mhe. Chiku Gallawa na Katibu Tawala Mkoa Bw. Salum Mohamed Chima.
 Baadhi ya wajumbe wa kikao wakisiliza kwa makini
 
 


Written by

0 comments: